Latest Updates

SAD NEWS: NESI MUHIMBILI AKATWA MIGUU, KISA?! SOMA ZAIDI HAPA!

Flora Nathaniel Shayo (60) mkazi wa Chanika, wilayani Ilala, Dar ameiomba serikali pamoja na Rais Jakaya Mrisho Kikwete imsaidie baada ya kukatwa miguu kutokana na kuugua ugonjwa wa kisukari.



Flora Nathaniel Shayo akatwa miguu baada ya kuugua kisukari. ILIKUWAJE?
Akizungumza na waandishi wetu hivi karibuni, Flora alisema aliwahi kuwa muuguzi (nesi) katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa miaka 26 iliyopita na baada ya kustaafu alikuwa akifanya biashara ya kuuza dawa za binadamu (Duka la dawa)huku mwanaye akiwa anafanya kazi za muziki.

Mama huyo aliendelea kufunguka kuwa, aligundulika kuwa na ugonjwa wa kisukari na presha mwaka 2006 ndipo akaanza kutumia dawa.

CHANZO CHA UGONJWA
Akifafanua zaidi mama huyo alikuwa na haya ya kusema: “Mwaka 2011 kidole gumba cha mguu wangu wa kulia kilianza kukauka na kubadilika rangi nikaenda Hospitali ya Taifa Muhimbili.

“Nilipofika hospitali nilipimwa na kugundulika kuwa sumu imepanda mpaka juu karibu na goti, madaktari wakaniambia ni lazima nikatwe mguu ili kuokoa maisha yangu. Nilipatwa na woga, lakini sikuwa na la kufanya, nilikubali.

“Nikaandaliwa na kupelekwa katika chumba cha upasuaji na kukatwa mguu, nilikuwa siamini kama kweli nimekuwa kilema lakini ilinibidi niamini, kweli hujafa hujaumbika,” alisema mama huyo huku akiwa na majonzi.

“Tangu nimekatwa mguu wa kwanza nateseka, mwanagu Dogo Mfaume ambaye ni mwanamuziki hana uwezo wa kunisaidia kutokana na ukweli kwamba hana kipato cha kutosha,” alisema huku akilengwalengwa na machozi.


Flora Nathaniel Shayo kabla ya kukatwa miguu. AKATWA MGUU WA PILI
Akasema: “Haukupita muda mrefu mguu wa pili nao ukaanza kuvimba, nilihisi kuchanganyikiwa na nikaona kuwa huo sasa ndiyo mwisho wa maisha yangu.

“Kwa kweli nilipatwa na msongo wa mawazo na kukata tamaa ya kuendelea kuishi baada ya kwenda tena Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na madaktari kuniambia mguu wa pili nao ukatwe, nilikatwa, namshukuru Mungu nimeuguzwa na kidonda kilipona vizuri lakini baada ya hapo nahisi akili yangu ilihama kabisa maana nilikuwa nahesabu siku za kuishi tu.

“Hakika mganga hajigangi. Sion thamani ya kuishi hapa duniani, nimebaki mkiwa na kujiona nastahili kufariki dunia maana sijui hata muelekeo wa maisha yangu utakuaje.”

OMBI KWA WATANZANIA
Baada ya kujifuta machozi kwa kanga yake aliendelea kusema: “Nawaomba Watanzania wenzangu wanisaidie kunichangia ili niweze kupata kiti cha magurudumu (wheelchair) kitakachoniwezesha kutoka nje na kufanya shughuli zangu.

“Ikiwezekana wanisaidie nipate miguu ya bandia, maana nashindwa hata kwenda nyumba ya ibada kusali au kufanya shughuli ndogondogo wakati bado nina nguvu kabisa ya kujitafutia riziki na kujenga taifa langu.”

OMBI KWA RAIS
Alimgusa Rais Kikwete huku akitiririka machozi akasema: “Namuomba Rais Kikwete aniangalie kwa kuwa nilifanya kazi Muhimbili kwa muda mrefu na pesa niliyoipata baada ya kustaafu haikuweza kukimu mahitaji yangu mpaka sasa nimebaki kama yatima tu.


Akikabidhiwa cheti baada ya kuhitimu kozi ya unesi. “Watoto wangu hawana uwezo na msaada nilioupata hospitali ni wa matibabu tu pale nilipohitajika kukatwa mguu, nahitaji dawa za kila siku, chakula na mahitaji mengine na dawa za kisukari ni gharama sana, kuna wakati nakosa hata pesa ya kununulia kwani presha pia inanisumbua.”

ATOA NENO KWA WASANII
“Kwa kuwa mwanangu Dogo Mfaume ni msanii, nawaomba rafiki zake na wasanii wenzake wanisaidie kwani hali niliyonayo ni mbaya, mpaka sasa naishi tu kwa matumaini. Kuna siku nakosa hata hela ya kwenda kujitibu,” alisema mama huyo kwa uchungu.

Naye Dogo alipotafutwa kuzungumzia ishu hiyo alisema, kwa sasa mambo yake hayapo sawa ndiyo sababu anashindwa kukidhi mahitaji ya mzazi wake.

“Kusema kweli hali ya mama inaniumiza sana kichwa, nashindwa hata kuelewa cha kufanya, nashindwa kumudu mahitaji yake ipasavyo ni tatizo kikubwa ningependa kwa yeyote ambaye yupo tayari kumsaidia basi asisite, siku zote mimi namuombea kwa Mungu mzazi wangu,”alisema Dogo Mfaume.

Yeyote aliyeguswa na habari hii na angependa kumsaidia awasiliane na mama huyu kwa namba 0755 216 865, kutoa ni moyo, sioyo utajiri.